Nahodha ambaye aliunga mkono mfumo wa Serikali mbili, alisema uwepo wa mambo mengi ndiyo unaoleta mkanganyiko.
Alisema hayo wakati akichangia maoni
kuhusu Katiba mpya mbele ya Tume ya kusikiliza Maoni iliyokutana jana na
wajumbe wa Baraza la Wawakilishi mjini hapa.
Katika mkutano huo ambao asilimia kubwa
ya wajumbe wote walizungumzia suala la Muungano pekee, Nahodha
alipendekeza masuala mengine yote yaondolewa kwenye Muungano ubakiwe na
ulinzi, polisi, uraia, mambo ya nje, sarafu, anga na usajili wa vyama
vya siasa.
Alisema kwa kuondoa mambo hayo, Bunge la
sasa lifanyiwe mabadiliko na liwe na sehemu mbili, ya kwanza
itakayozungumzia mambo manane ya Muungano na ya pili izungumzie masuala
ya Tanzania Bara.
Aidha, aliendeleza maoni ya kutaka uwepo
utaratibu wa kupokezana urais kati ya Bara na Zanzibar kwa kipindi cha
kila baada ya miaka ya 10.
“Wengine tunapoeleza hivyo wanapata
wasiwasi wanadhani tunataka kupata rais substandard (chini ya viwango),”
alisema Nahodha na kusisitiza kwamba vigezo na sifa viwe vile vile kama
vilivyopo.
Kuhusu mgawanyo wa mapato, alisema suala
hilo limebaki kuwa la kutupiana mpira kutokana na tatizo kwamba
halikuwekwa kwenye Katiba.
Waziri huyo aliyewahi kuwa Waziri
Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), alipendekeza Zanzibar
ipewe asilimia 15 ya mapato ya vyanzo vyote vilivyo kwenye Muungano na
itajwe kwenye Katiba.
“Mwanzo waliangalia idadi ya watu kwamba
uwiano wa watu wa Zanzibar ni 3.5 wakasema mapato ya Zanzibar ni kama
asilimia nne,” alisema na kusisitiza kwamba vigezo hivyo si sahihi kwa
kuwa Serikali ina jukumu sawa na bara la kuhudumia watu wake.
Nahodha ambaye alisema Zanzibar
imepoteza mamlaka yake ikiwa ni pamoja na kupoteza uwezo wa kupata
misaada kutoka nje ikiwemo OIC, aliendelea kusema, “Zanzibar ilipounda
Muungano tumepoteza mamlaka ya kushirikiana na nchi za nje… hivyo hiyo
asilimia 15 ni sawa na kulipwa fidia,” alisema.
Wengine waliochangia ni Mwakilishi wa
Chumbuni, Machano Othman Said (CCM) alipendekeza Muungano uliopo
uendelee, lakini akataka katika Katiba ijayo, Rais wa Zanzibar awe
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano.
Mwakilishi wa Jimbo la Chonga, Abdalah
Juma Abdalah (CUF) alipendekeza mfumo wa Muungano wa mkataba maalumu
chini ya utaratibu maalumu ambao kila upande unakuwa huru kupunguza
jambo litakaloonekana halina maslahi kwake.
Naye Mwakilishi wa Tumbe, Rufai Said
Rufai (CUF) pamoja na kupendekeza Zanzibar na Tanganyika kila moja iwe
na mamlaka yake kamili kwa lengo la kuunda Muungano wa mkataba, alitaka
Wabara wanaoishi visiwani na Wazanzibari walioko Bara, wawe na hiari ya
kuishi wanakotaka bila kubughudhiwa.
Comments
Post a Comment