NI SIMBA AMA YANGA? UWANJA WA TAIFA LEO HII

VPL_LOGOWakati leo Vigogo wa Soka na Mahasimu wakubwa, Simba na Yanga, zinatinga Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kucheza Mechi yao ya kwanza ya Ligi Kuu Vodacom, tayari utata umeshaanza kuigubika ‘BIGI MECHI ’ hiyo baada ya Simba kusema imeshtushwa na kushangazwa na uteuzi wa Refa wa Mechi hiyo uliofanywa na Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, kwa kumpanga mfululizo Refa Mathew Akrama wa Mwanza.
Akiongelea ishu hiyo ya Refa, Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema kuwa Akrama alichezesha Mechi ya Jumapili ya Yanga na African Lyon ambayo Yanga walishinda bao 3-1 na wanashangaa leo tena ameteuliwa kwenye Mechi ya Simba na Yanga.

Hata hivyo, Kamwaga alifafanua: “Hili limetushangaza sana, lakini hatuna tatizo ila tunamtaka achezeshe kwa kufuata haki maana ile mechi kuna watu wanaweza kufa kwa presha, wengine wameweka rehani nyumba zao na vitu mbalimbali hivyo si mchezo wa utani. Tunamsihi afuate sheria hatutaki apendelee timu ya aina yoyote, sisi tunataka matokeo ya uwanjani kama tukifungwa na yeye amechezesha vizuri tutakuwa wa kwanza kumpongeza.“
Mara ya mwisho kwa Yanga na Simba kukutana ilikuwa ni Mei 6 Mwaka huu katika Mechi ya mwisho ya Msimu wa 2011/12 ambayo Simba iliicharaza Yanga bao 5-0 na kutawazwa rasmi Mabingwa wa Tanzania Bara.
Pia, kipigo hicho ndicho kiliangusha himaya ya Uongozi wa Yanga wa Mwenyekiti Lloyd Nchunga na kupelekea kufanyika Uchaguzi mdogo uliomsimika Mfadhili mkuu wa Klabu hiyo, Yusuf Manji, kuwa ndio Mwenyekiti mpya.
Kwa sasa, tangu Ligi Msimu huu ianze, Simba imekuwa na matokeo mazuri kwa kushinda Mechi zao zote 4 na wapo kileleni wakiwa na Pointi 12 wakati Yanga wameanza kwa kusuasua ikiwa na Pointi 7, ikiwa nafasi ya 6, kwa kushinda Mechi mbili, kufungwa moja na kutoka sare moja.
Matokeo hayo yameifanya Yanga imtimue Kocha wao Tom Saintfiet na kumwajiri Mholanzi Ernie Brandts aliewasili Nchini Ijumaa iliyopita lakini kwa sasa jukumu la kuifundisha Yanga limekuwa chini ya aliewahi kuwa Mchezaji wao mahiri Fred Felix Minziro.
Simba, chini ya Kocha Mkuu Mserbia Milovan Cirkovic, itatinga Uwanjani bila Nyota wao wawili, Emmanuel Okwi na Amir Maftah, ambao wanatumikia Vifungo baada ya kulimwa Kadi Nyekundu hivi karibuni.
Hata hivyo, Simba bado inao Wachezaji wakali, wakiongozwa na Kipa mkongwe Juma Kaseja, ambao ni kina Felix Sunzu toka Zambia, Mghana Daniel Akuffor, Mrisho Ngassa , Chipukizi Edward Christopher, Mwinyi Kazimoto na Ramadhan Chombo ‘Redondo’.
Nao Yanga inao Wachezaji wa kutisha kina Hamisi Kiiza toka Uganda, Mrundi Didier Kavumbagu, Said Bahanunzi, Simon Msuva, Athumani Idd ‘Chuji’, Haruna Niyonzima, Frank Domayo, Kelvin Yondani, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ pamoja na Mbuyu Twite.
VIKOSI VINATARAJIWA:
Yanga: Yaw Berko, Mbuyu Twite, Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kelvin Yondani, Athuman Idd ‘Chuji’, Frank Domayo, Haruna Niyonzima, Didier Kavumbagu, Hamisi Kiiza, Simon Msuva.
Simba: Juma Kaseja, Nassoro Masoud, Paul Ngalema, Juma Nyosso, Shomari Kapombe, Jonas Mkude, Mwinyi, Kazimoto, Amri Kiemba, Felix Sunzu, Edrward Christopher, Mrisho Ngassa.
VIINGILIO:
Kiingilio cha chini ni sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya kijani ambavyo ni 19,648 kwenye uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 60,000. Watazamaji watakaoketi kwenye viti vya rangi ya bluu ambavyo ni 17,045 watalipa sh. 7,000 kwa tiketi moja.
Sh. 10,000 ni kwa viti vya rangi ya chungwa ambavyo viko 11,897 wakati VIP C inayochukua watazamaji 4,060 itakuwa sh. 15,000. Kwa upande wa VIP B tiketi ni sh. 20,000 na VIP A yenye watazamaji 748 tu kiingilio kitakuwa sh. 30,000.
WAAMUZI:
Refa: Mathew Akrama kutoka Mwanza
Refa Wasaidizi: Samuel Mpenzu kutoka Arusha, Ephrony Ndissa wa Dar es Salaam
Refa wa Akiba: Oden Mbaga wa Dar es Salaam.

Comments